UMUHIMU WA MAOMBI KATIKA IBADA

MAOMBI
Haya ni mawasiliano kati yako na Mungu wa Mbinguni.Na kama ilivyo kwa mawasiliano ya kawaida mfano ya moja kwa moja, ya simu, ya barua au kwa njia nyingine yoyote maombi lazima yawe ni majibizano(dialogue) kati ya watu wawili au zaidi.Kama nilivyo sema katika sura zilizopita kuwa Mungu anataka kuwe na mazingira yanayofaa(condunsive environment) ili mtu aweze kumwabudu Mungu kwa Roho na kweli, hivyo vitu vyote tunavyohitaji, Mungu ameshaviandaa katika ulimwengu wa Roho,uwe utajiri, elimu, mke au mume, chakula, afya, mahali pa kuishi, kazi na mengine yote.Hivyo, tafsiri nyingine ya maombi ni kuchukua vitu katika ulimwengu wa roho na kuvibadilisha viwe katika ulimwengu wa mwili.Lazima utambue kila unachokiomba kipo katika ulimwengu wa roho na inakuhitaji wewe uingie kwenye maombi ili ukibadilishe kiwe katika ulimwengu wa mwili(halisi).

Ndio maana wakati mfalme Hezekia alipokuwa akiongoza wana wa Israeli ilifikia wakati Mfalme wa Ashuru alianza kuwadhihaki na kuwatukana siyo kwa sababu Mungu hakuwepo au ushindi haukuwa wao, lakini Mungu alitaka wapitie hatua ya maombi kuomba ushindi katika ulimwengu wa roho udhihirike kwa namna ya mwili.Tunasoma Isaya 37;3, “Wakamwambia, Hezekia asema hivi,Siku hii ni siku ya dhiki, na aibu na matukano; maana watoto wa tayari kuzaliwa, wala hapana nguvu za kuwazaa”.Maana yake hakuna kitu kinachoweza kufanya watoto wazaliwe ingawa ndani ya tumbo wamo.Kuna watu wengi hupata mafunuo ya aina mbalimbali kuhusu maisha yao ya mbele au ya wengine lakini mara nyingi hayo mafunuo hayatokei kama yalivyo au hayatokei kabisa sababu ni kwamba haukuingia kwenye maombi kwani yalikuja kwa namna ya roho na wewe ulitakiwa uyalete katika ulimwengu wa mwili yadhihirike.

Dada mmoja aliniambia kuwa siku mbili kabla mama yake hajafariki aliota ndoto kuhusu kifo hicho.Akabaki tu na hofu na huzuni kusubiri hicho kifo baada ya siku hizo mbili mama yake akafa.Sasa hii ni hatari sana unapopewa maono au ufunuo wa namna hii maana yake wajibu wako ni kuomba hiyo roho ya mauti isiwe na nguvu juu yake ili apewe uzima na aendelee kuishi.Na lazima unapoingia kwenye maombi uhakikishe hautoki mpaka kitu unachoomba kinatokea(PRAY  UNTIL  SOMETHING  HAPPEN).Katika kuomba kwako utakapoomba sawasawa Mungu atakupa mwongozo wa nini cha kufanya ili ukipate kile unachokihitaji.Wakati mwingine Mungu anakuwa amekuchagua wewe pekee ili usimamie kwa njia ya maombi kitu Fulani kitokee au kitu Fulani kisitokee na unapokiuka na kuacha kuomba kama anavyokupa mwongozo ujue unavuruga mfumo mzima wa kufanyika au kutokufanyika kwa hicho kitu iwe kinakuhusu wewe au mtu mwingine lazima uwe makini sana.
Kumbuka pia maombi yako ni kama manukato(pafyumu) mbele za Mungu unapoomba, maana yake katika ulimwengu wa roho unafanya hali ya hewa ya mbinguni iwe nzuri na kupendeza. “Hata alipokitwaa kile kitabu, hao wenye uhai wanne na wale wazee ishirini na wanne wakaanguka mbele za mwanakondoo, kila mmoja wao ana kinubi, na vitasa vya dhahabu vilivyojaa manukato ,ambayo ni maombi ya watakatifu”.Ufunuo 5;8.Wakati mwingine inatokea Baraka zinashuka juu ya nchi au familia lakini uliomba tu kwaajili ya mambo mengine ya ufalme wa Mungu. Maombi yako yanamgusa Mungu lakini endapo unaomba kwa utakatifu.

NAFASI YA ROHO MTAKATIFU KATIKA MAOMBI YAKO
Roho mtakatifu ni nafsi ya tatu ya Mungu ambapo nyingine ni Mungu Baba na Mungu mwana(Yesu).Katika kila kipindi Mungu amekuwa akidhihirika kwa watu wake kwa namna mbalimbali.Katika Agano la kale Mungu amekuwa akidhihirika kwa nafsi ya kwanza ya Mungu Baba.Hii tunaiona dhahiri wakati akisema na Adamu,Nuhu, Ibrahimu, Musa, Eliya na wengine.Katika Agano jipya kabla ya siku ya Pentekoste, Mungu amekuwa akidhihirika kwetu kwa nafsi ya pili ya Mungu mwana(YESU) ndio maana wakati Yesu anatarajiwa kuzaliwa malaika akamwambia Bikira Mariamu, “Hayo yote yamekuwa ili litimie neno lililonenwa na BWANA kwa ujumbe wa nabii akisema, Tazama, Bikira atazaa mwana; Nao watamwita Imanueli; Yaani Mungu pamoja nasi”.Mathayo 1;22-23.
Kazi yake Yesu ilikuwa kufanya matengenezo na urejesho wa mwanadamu kwa Mungu na kumwandaa mwanadamu ili aweze kukaa ndani yake.Sasa baada ya Yesu kufanya kazi yake aliyotumwa ikawa ni zamu ya Roho mtakatifu nafsi ya tatu ya Mungu kuja kukaa na mwanadamu na kudhihirika mpaka mwisho wa dunia.Pasipo Roho mtakatifu sisi hatuwezi kamwe kuomba itupasavyo. “Kadhalika Roho naye hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo; lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa”.Warumi 8;26.Hivyo wakati wote ili maombi yetu yapate kibali mbele za Mungu ni lazima Roho Mtakatifu atuongoze kuomba.Yeye anafanya kazi ya kushuhudia kwa ulimwengu(wasiookoka) juu ya dhambi, haki na hukumu (Yohana 16;8-11).Na kwetu sisi ambao tumeokoka Yesu anasema, “Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli,atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayo yasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake”.Yohana 16;13.Pia anasema katika Yohana 14:26, “Lakini huyo msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwenu kwa jina langu, atawafundisha yote na kuwakumbusha yote niliyowaambia”.
Anaposema atawafundisha yote maana yake hata kama biashara, masomo, ndoa, uchumba, au lolote lile linakutatiza yeye anaweza kukufundisha.Roho Mtakatifu anapokuwa ndani yako hata pumzi yako inakuwa tofauti, inakuwa kama ya Mungu na inakuwa na nguvu sawasawa kabisa na ya Mungu kwani Roho Mtakatifu yumo. Maana yake ukiwapulizia wagonjwa wanapata afya,hata mtu aliyekufa anafufuka.Kumbuka kwa pumzi hiyohiyo Mbingu na nchi zilifanyika(Zaburi 33;6) na kwa pumzi Mungu alimpulizia mtu naye akawa nafsi hai(Mwanzo 2;7).Biblia inasema, “Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake”. Warumi 8;28.Mungu anataka afanye kazi na wewe katika kuwafanya watu wapate afya na ufufuko miilini mwao.
Kuna mambo mawili yanayofanya pumzi yako isipitishe NGUVU za Mungu au isifanye kazi kama Mungu alivyokusudia.Jambo la kwanza ni kutokufahamu juu ya inatokea nini unapomruhusu Roho Mtakatifu atende kazi kupitia pumzi yako.Jambo la pili ni kutia unajisi katika njia au mfumo ambao pumzi hiyo inapitia.
Yesu anasema, “Yeye aniaminiye mimi kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam na kubwa kuliko hizo atazifanya: kwa kuwa mimi naenda baba”.Yohana 14;12.Anaposema, “kwa kuwa mimi naenda kwa Baba” ,kwa maana nyingine ni kuwa kwa kuwa Roho Mtakatifu atawashukia na kukaa nanyi.Ndio maana alisema yawafaa ninyi mimi niondoke maana nisipoondoka huyo msaidizi(Roho Mtakatifu) hatakuja kwenu(Yohana 16;7).Hivyo ili ufanye kazi kubwa na miujiza mikuu kwa ajili ya utukufu wa Mungu ni lazima uwe na Roho mtakatifu ndani yako na umpe nafasi ya kutosha kabisa ili aweze kuonesha ukubwa wa uweza wake usio na mwisho katika kutenda miujiza.


KUNENA KWA LUGHA.
Kunena kwa lugha ni matokeo au ishara mojawapo ya wazi ya kuwepo kwa Roho Mtakatifu ndani yako.Na hii haimaanishi kuwa usiponena kwa lugha basi moja kwa moja hauna Roho Mtakatifu, La hasha!!Matendo ya mitume 2;4, “wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine kama Roho alivyowajalia kutamka”.Pia mtume Paulo anasema katika 1Wakorintho 14;2, “Maana yeye anenaye kwa lugha,hasemi na watu bali husema na Mungu; maana hakuna asikiaye; lakini anena mambo ya siri katika roho yake”.Hivyo ni muhimu sana kwa uliyejazwa na Roho Mtakatifu uwe na kiu na unene kwa lugha kwani ni Roho Mtakatifu anakuwa anazungumza mwenyewe mbele za Mungu ule uhitaji halisi wa roho yako..Saa nyingine unaponena kwa lugha unakuwa unaombea au kutamka hata mambo ambayo yako juu ya kiwango cha imani yako lakini yanakuwa yako katika mapenzi ya Mungu uyapate kwa wakati huo.Kwa tafsiri nyingine  tunaweza kuita MUUJIZA.Unapoomba kwa kutumia akili mara nyingi utaomba juu ya mambo yale uyajuayo tu. Wakati mwingine kunakuwa na jambo baya ambalo litatokea mbele yako mfano Ajali, kifo, kufukuzwa kazi, nyumba kuungua moto, hitilafu ya umeme n.k  na unakuta ndani yako unapata msukumo wa kuomba lakini hujui uombe au uombee juu ya nini lakini kunena kwa lugha kunakusaidia  uweze kuomba  au kuombea hilo tukio mbele yako na kulizuia mapema lisitokee.

Jambo la muhimu la kujua ni kuwa kunena kwa lugha siyo ufahamu au ujuzi anaokuwa nao mtu wa kuomba bali ni neema ya bubujiko la Roho Mtakatifu.Hivyo, omba Mungu akupe kiu hii kubwa baada ya kutambua umuhimu wa kunena kwa lugha ili uombe kama vile Mungu atakavyo uombe na wala usijaribu kuigiza maana utakuwa umemdharau Roho mtakatifu ambaye ndiye mpaji na hapohapo utafanya shetani apate mwanya wa kukuingizia lugha bandia za mapepo.Kumbuka kuna lugha mbalimbali kama vile za watu, wanyama, malaika, mapepo n.k. hivyo pia ni lazima uwe makini. Kunena katika Roho Mtakatifu lazima utajisikia huru, mwepesi na pia utasikia amani ya Mungu ndani yako.

Nafasi ya kifalme na kikuhani katika maombi yako.
Kazi mojawapo ya KUHANI ni kuomba toba na utakaso kwa ajili ya watu au mahali Fulani.Wakati wote wa Agano la kale Mungu amewatumia makuhani katika maeneo yote yahusuyo toba au utakaso wowote ule.Nao ndio pekee walioruhusiwa kuingia patakatifu pa patakatifu sehemu ya ndani kabisa ya hekalu huku akiwa  amejitakasa yeye kwanza.Baada ya Yesu kuja Mungu akamfanya awe kuhani mkuu kwa Mungu wetu kwaajili ya dhambi zetu.
Maana ameshuhudiwa kwamba; wewe u kuhani milele, kwa mfano wa Melkizedeki……………………Na kwa kuwa haikuwa pasipo kiapo, (maana wale walifanywa makuhani pasipo kiapo bali yeye, pamoja na kiapo kwa yeye aliyemwambia ,Bwana amwapa wala hataghairi U kuhani milele;)basi kwa kadiri hii Yesu amekuwa mdhamini wa Agano lililo bora zaidi”.Waebrania 7;17-22.Ndio maana alipokuwa akikata roho msalabani pazia la hekalu  lilipasuka vipande viwili toka chini mpaka juu.Hii ilikuwa ishara ya kuachiliwa kwa wana wa Mungu (watakaookoka) kuingia patakatifu pa patakatifu kama makuhani.
MFALME ni mtu ambaye anatawala na kumiliki ufalme katika eneo Fulani.Na yeye ndiye mwamuzi wa mwisho katika hilo eneo.Maana yake akitaka kuzuia jambo Fulani baya au zuri linalotendeka mahali hapo anaweza wala hakuna awezaye kumzuia. “Kwakuwa neno la mfalme lina mguvu, naye ni nani awezaye kumwambia huyo, wafanya nini?”.Mhubiri 8;4.Mamlaka ya kifalme huwa inatoka kwa Mungu au kwa miungu mingine(shetani) ndio maana hata neno lake(mfalme) ni vigumu kulipinga au kuzuia.
Lakini mimi nizungumzie kwa upande wa Ufalme ambao unapewa kutoka kwa Mungu ambaye ni mfalme wa wafalme.Neno linalotoka kwa huo ufalme linakuwa na nguvu juu ya falme na kila mamlaka iwayo yote.
Msiogope enyi kundi dogo; kwa kuwa Baba yenu ameona vema kuwapa ule ufalme”.Luka 12;32.Hivyo fahamu wazi kuwa wewe ni mfalme na umepewa majukumu ya kifalme na Mungu mwenyewe.Na kiwango cha kutawala na kumiliki kieneo kinategemea maamuzi yako na utendaji wako wa kazi uliyopewa. Ufunuo 5;9-10 inasema, “……………….kwa kuwa ulichinjwa, ukamnunulia Mungu kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa, ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu,Nao wanamiliki juu ya nchi”.Sema tena “Ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu”. Ukikaa sawasawa katika nafasi yako ya kifalme na kikuhani unapewa uwezo wa kumiliki nchi yaani eneo husika lenye mipaka kamili.Hakuna haja ya kulalamika ooh!! nashindwa kuabudu kwani nyumba yangu ipo karibu na baa au klabu ya pombe, au hakuna haja ya kufanya mgomo ili upate haki au mshahara wako matokeo yake unapigwa na askari wa usalama na kuumia bure.Badala yake kaa na kutulia halafu chukua nafasi ya kikuhani kwa kuomba toba kwa ajili ya watu hao au eneo husika unalotaka hayo mabadiliko kisha, chukua nafasi ya kifalme kwa kutamka neno la kifalme la uamuzi wa mwisho ulioamua kwa mazingira hayo kuwepo kwa njia ya maombi na Mungu ni lazima atafanya mabadiliko.Usiombe kama vile mtu asiyestahili(mtumwa) kama mwanamke Mkananayo(Mathayo 15;21-28).Kwani Mungu amekustahilisha kuwa mtoto wake.Yesu akawaambia, “Siwaiti tena watumwa; kwa maana mtumwa hajui atendalo Bwana wake; lakini ninyi nimewaita rafiki; kwakuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu”.Yohana 15;15.
Wengine wanapoomba kwa ajili ya mtu mwenye mapepo wananyenyekea na kupiga magoti kwani hawajui nini wanakifanya lakini nakuambia katika kazi hiyo au maombi hayo hebu kemea pepo au nguvu za giza huku umesimama kwa ujasiri kabisa kama mfalme kwa mamlaka uliyopewa na BWANA nakuambia pepo atachomoka bila kuleta kiburi chochote kwani anajua unaifahamu nafasi yako uliyopewa na Mungu.

WITO.
Ikiwa umejifunza na kutambua sasa kuwa Ibada yako haikuwa sawa mbele za Mungu au bado ndani yako haujampokea Yesu kuwa ni Bwana na mwokozi wa maisha yako( HAUJAOKOKA) na unataka urudi kwenye msingi wa kumwabudu Mungu halisi katika Roho na kweli, haujachelewa.Yesu anasema, “Tazama nasimama, mlangoni, nabisha; mtu akiisikia sauti yangu, na kuufungua mlango, nitaingia kwake nami nitakula pamoja naye(mambo yote hatatenda bila kukushirikisha), na yeye pamoja nami”.Ufunuo 3;20.
Kwa maana husema, Wakati uliokubalika nalikusikia, Siku ya wokovu nalikusaidia; Tazama wakati uliokubalika ndio sasa; tazama siku ya wokovu ndiyo sasa”.2Wakorintho 6;2.
Tafuta MAHALI PA UTULIVU na Sema sala hii pamoja nami kwa Roho na kweli kutoka ndani ya moyo wako;
Bwana Yesu, ninakushukuru kwa Rehema na fadhili zako nyingi ulizozionesha pale ulipojitoa na kufa msalabani kwa ajili yangu mimi mwenye dhambi.Ninakuja kwako, ninaomba unisamehe dhambi zangu zote na unipokee,futa jina langu katika kitabu cha mauti, na uliandike kwenye kitabu cha uzima; unipe uwezo wa kufanyika mtoto  wako tangu sasa. Ninajiachilia kwako, uwe BWANA na mwokozi wa maisha yangu; unitawale katika mwili, nafsi na roho yangu, nikatembee katika mapenzi yako siku zote za maisha yangu.Asante kwa kuwa tangu sasa nimeokoka na kuwa kiumbe kipya. Ya kale yote yamepita na tazama,yamekuwa MAPYA, katika jina lenye NGUVU na MAMLAKA, jina la YESU ninaomba na kuamini kuwa nimepokea sasa.AMEN!!!
Baada ya kusema sala hii amini kuwa upo ndani ya Yesu naye yuko ndani yako.Endelea kuishi katika misingi ya utakatifu katika kujifunza Neno lake na maombi huku ukiufurahia UZURI wa Yesu usiochakaa ndani ya wokovu huu aliokupa.Anasema, “ na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote hata ukamilifu wa dahari”. Mathayo 28;20b.      MUNGU AKUBARIKI!!!!


Kwa maombezi, maswali, maoni, ushauri au kama unaguswa kuwa mwombezi maalumu kwa huduma hii, tafadhali usisite kuwasiliana nami kwa anuani zifuatazo;
Simu namba; 0757 350 527 au 0717 236 490.

Comments

Popular posts from this blog

NAMNA YA KURUHUSU UTUKUFU (GLORY) WA BWANA KUFANYA JAMBO KATIKA MAISHA YAKO