SIFA.
Maana halisi ya sifa ni kumwambia au kumshuhudia Mungu au watu matendo ambayo huyo Mungu wako ameyafanya.Hii inatokana na mguso wa ndani ya moyo wa mtu unaompelekea aimbe kwa furaha, acheze, arukeruke na kushangilia huku akimtaja Mungu wake na matendo ambayo ametendewa.Inawezekana ikawa uhai, kuponywa magonjwa, kupewa nafasi nzuri kimasomo, kupata kazi, kuinuliwa kiroho, kusamehewa n.k.Sifa ipo katika maeneo makuu mawili ambayo ni sifa ya Mungu aliye hai au sifa kwa mashetani.

Nikianza na sifa ya Mungu biblia inasema; “Haleluya, Msifuni Mungu katika patakatifu pake, Msifuni katika anga la uweza wake, Msifuni kwa matendo yake makuu;Msifuni kwa kadiri ya wingi wa ukuu wake…………………………….Na kila mwenye pumzi na amsifu BWANA. Haleluya!”.Zaburi 150:1-6.Anaposema msifuni Mungu katika patakatifu pake maana yake ni Mbinguni,mbele ya kiti chake cha enzi au pamoja naye; ndio maana nimekwambia lazima uwe mtakatifu kwa sababu ndipo mahali pa kumpa Mungu sifa pekee.Mungu wetu ni mtakatifu, anakaa mahali patakatifu na lazima vyote vilivyopo karibu naye viwe vitakatifu.Kutoka 19:110-21.

Unapokuwa katika sifa hebu sifu kama upo mbele ya Bwana mwenye NGUVU na UWEZA, usisifu kizembekizembe.Ndio maana anasema msifuni Mungu katika anga la uweza wake, kwa matendo yake makuu na kwa kadri ya wingi wa ukuu wake.

Wakati ule mfalme Daudi ameshinda ile vita na Wafilisti hakujali nafasi yake kama mfalme maana alijua kuna mfalme wa wafalme anayemsifu ambaye ndiye hasa aliyefanya washinde na warudi na sanduku la Agano.Na Yule mwanamke aliyetaka mfalme asisifu kwa jinsi ile alipata laana ya kutopata mtoto maisha yake yote.(2Samweli 6:16,20-23).Usijaribu kuzuia sifa itokayo ndani ya mtu kwaajili ya BWANA maana hakika laana itakuwa juu yako.Sifa ya Mungu ni ya Mungu wala hakuna mtu awezaye kuchukua sehemu yake.

Kwa upande wa sifa ya shetani watu huingia kumsifu shetani, maovu na kazi nyingine anazofanya.Pia wengine husifu dhambi kuwa ni kitu kizuri kufanya na ndio maana usishangae unapoona karibu asilimia tisini (90%) ya vijana wanaoimba nyimbo za kidunia wanaimba juu ya suala la mapenzi au zinaa wakati Mungu kasema wazi kuwa usizini wala kumtamani mwanamke(au mwanamume) asiye wako.Kinyume chake unakuta anaimba na mtu asiye wake  na kuanza kukumbatiana na kufanyiana vitendo vya uzinzi halafu baadaye utamkuta na mtu mwingine akiimba na kufanya mambo yaleyale.Hii ni kukaribisha Sodoma na Gomora nyingine kwa mara ya pili.
Biblia inasema, “Wala msiifuatishe namna ya dunia hii, bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu, yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu”.Warumi 12:2.

Sasa watu wengi wamekuwa wakiiga mitindo/staili za muziki ya kidunia na kuingiza katika kumwabudu Mungu na makanisa mengi sasa hivi yamejaa machafuko haya.Na wengi hujidanganya na kujifariji kuwa wananyang’anya kile ambacho shetani alidondoka nacho kutoka Mbinguni.Lakini Biblia inasema, “Hivyo husema, Alipaa juu aliteka mateka, Akawapa wanadamu vipawa”.Waefeso 4;8   .Maana yake ujuzi au kipawa unapewa kutoka juu yaani Mbinguni na sio kwingineko.Sasa inashangaza kwako kusubiri ujuzi ambao shetani anawafunulia watu wake ndipo uige.Hebu kaa utulie halafu umwambie Mungu nahitaji kukusifu kwa ustadi zaidi, naomba unipe ujuzi, na Mungu sio dhalimu hata akashindwa kukupa,atakupa tu.

Tambua hii siri kuwa kila alama unayoijua ina maana yake au kazi yake na hiyo kazi inaweza kuwa nzuri au mbaya.Kwa mfano mstari(                ) ni nukta iliyoendelezwa.Kuna watu hunishangaza wanapojiita majina ya ajabu mfano, “RED DEVIL” na wala hawana shida pasipokujua kuwa wanamtukuza shetani na kuwa kuna madhara yake tena makubwa, halafu na wewe mtu wa Mungu huoni shida hata kidogo na unashangilia tu!!shauri yako, Mungu anaweza kukutapika.Au unafahamu ni kwanini waimbaji wengi wa muziki wa kidunia wanaimba huku wanachomachoma mikono yao chini(kuzimu) na huku watu wa Mungu wakiabudu wanaelekeza mikono yao juu (Mbinguni)?

Wengi hawajui wanachokifanya lakini ninakuambia wazi kuwa wanamwabudu Shetani kama Mungu bila kujijua.Unakuta wanapoimba vibwagizo vyao ni, “yo!yo!yo!” au “G!G!G!” n.k.Hivi vitu au maneno vina maana kabisa na kazi yake.Hebu omba Mungu akufunulie zaidi na kukuelewesha juu ya mambo hayo ili upate ufahamu na maarifa.

Hosea 4:6, “Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa; kwa kuwa wewe umeyakataa maarifa, mimi nami nitakukataa wewe, usiwe kuhani kwangu mimi, kwa kuwa umeisahau sheria ya Mungu wako, mimi nami nimewasahau watoto wako”.Lazima ukifahamu kile unachokifanya kama ni cha Mungu au cha kishetani kwa kumuuliza Mungu.Mtumishi mmoja alisema hivi, “Je, huwa unafanya nini unapokuwa hujui nini cha kufanya?”.Jawabu ni kwamba lazima umuulize Mungu, usiingie kufanya halafu baadaye ukapata madhara makubwa.

Siku moja nikiwa nimelala niliota ndoto hii; “ nilikuwa na rafiki yangu mmoja mahali Fulani baada ya kuzungumza naye kitambo akaniambia twende pamoja nikachukue kitu fulani nyumbani kwao.Tulipita kwenye nyumba moja ambapo mimi nilipita nyuma ya ile nyumba na yeye mbele yake.Baada ya kuivuka nikakuta Yule mwenzangu yuko mbele umbali kidogo, nikajipa matumaini kuwa nitamkuta tu.Nikafika sehemu kuna nyumba nyingine halafu kwa pembeni kuna msitu mkubwa.Nikawa nasikia kama kuna sauti za watu waimbao.Nikamuuliza mmoja wa wakazi wa pale, kuna nini kinaendelea huko msituni? Akasema katikati ya huo msitu kuna kanisa liitwalo “NGUVU YA NGOMA”.Nikageuka kutazama kwenye mlango(mwanzo wa kuingia ndani ya huo msitu) na nikaona kuwa kulikuwa  na miti ambayo juu yake kulikuwa na majitu na kamba imeteremshwa mpaka chini, na kila apitaye ananaswa na kamba na kupandishwa juu.Nilikuwa na wazo la kuingia nione wanaabuduje lakini nilipoona mtu mmoja amenaswa anapandishwa juu na kamba nikaogopa.Ghafla nikajikuta nipo nyuma ya hilo kanisa nyuma kabisa na wakati huo watu wote walikuwa mbele wanasifu na mdundo mzito wa ngoma.Wengi wao walikuwa watoto na vijana pia baadhi ya wazee walikuwepo.Roho wa Mungu akaniambia hilo ni moja ya makanisa yanayotolewa kuzimu na kuletwa duniani.Lengo ni kuwateka watu hasa watoto na vijana kwa njia ya sifa(uimbaji) waingie jehanamu”.

Ninapenda nikwambie kuwa sifa halisi ina NGUVU kubwa na ya ajabu.Maana yake ukimsifu Mungu utaona nguvu za Mungu hali kadhalika ukimsifu shetani utapata nguvu zake.Inashangaza ninapoona watu(vijana) wanaimba nyimbo na kusema, “Nakupenda mpenzi jini” au “nataka niolewe na jini” sijui wanaelewa maana yake au wanaimba kwa lengo la kuwafurahisha
watu.Ni ajabu hasa ninapoona hata mtu uliyeokoka unajiingiza huko na hapo ni lazima Ibada yako ivurugike hata ukatae!!

MJUE SHETANI NA MBINU ZAKE

Kabla ya kuasi kwake shetani alikuwa ni malaika mkuu wa sifa mbinguni na jina lake akiitwa Lusifa. “Ulikuwa ndani ya Adeni, bustani ya Mungu; kila jiwe la thamani lilikuwa kifuniko chako……………………….kazi ya matari na filimbi ilikuwa ndani yako; katika siku ya kuumbwa kwako zilitengenezwa tayari.Wewe ulikuwa Kerubi mwenye kutiwa mafuta afunikaye; nami nalikuweka hata ukawa juu ya mlima mtakatifu wa Mungu, ukatembea huko na huko kati ya mawe ya moto.Ulikuwa mkamilifu katika njia zako tangu siku ulipoumbwa, hata uovu ulipoonekana ndani yako”.Ezekieli 28:13-15.

Baada ya kuasi jeshi la Mbinguni wakamtupa chini kuzimu pamoja na malaika waliokuwa wameungana naye. “………………….Lakini utashushwa mpaka kuzimu mpaka pande za mwisho za shimo”.Isaya 14:14-15.Baada ya hapo shetani akaanza mikakati mikubwa ya kuhakikisha mwanadamu naye anaangamia pamoja naye kwenye moto wa milele.Kwa kuanza na baba yetu Adamu akaanza kupanua mtandao na mbinu mbalimbali.Moja ya mbinu pekee ambazo shetani anatumia ni kupitia uimbaji (MUZIKI) ili watu wamsifu au wapotoshane wao kwa wao na kuzama kuzimu.

Kwa mfano katika  miaka iliyopita kuna mwimbaji aliimba wimbo mmoja usemao “IN DEMON” yaani “NDANI YA SHETANI”.Katika kipindi hicho wimbo huo uliteka watu wengi sana.Lengo lake kuu ni watu wawe kwenye miliki yake(shetani).Ogopa sana kumkaribisha shetani kwa jinsi hiyo kwenye Ibada yako siku zote.
Kumbuka mfalme Herode alikuwa ni mtu aliyempenda sana Yohana mbatizaji lakini katika sherehe yake baada ya kupigwa mziki( nyimbo za kidunia ) na binti yake kucheza sana akaingia kufanya maamuzi kinyume na mapenzi ya Mungu na yeye mwenyewe ya kumkata kichwa Yohana mbatizaji.Hii ni kutokana na uwepo wa kishetani uliokuwa umejaa pale kwa sababu ya nyimbo zile.





FAIDA ZA SIFA YA KIMUNGU.

                  i).Kufunguliwa na kuachiliwa huru.
Wakati ule Paulo na Sila walipokuwa wakihubiri INjili kwa nguvu sehemu nyingi na kufanya miujiza ya pekee hasa walipomfungua Yule kijakazi mmoja aliyekuwa na pepo la utambuzi, walikamatwa kwa kuteswa na kufungiwa gerezani na wale walinzi wakaamriwa wawalinde sana.Lakini panapo usiku wa manane Paulo na Sila wakakumbuka siri iliyomo katika kufanya ibada hususani katika eneo la kusifu, wakawa wakimwomba Mungu na kumwimbia nyimbo za kusifu, na mara tetemeko kuu la nchi likatokea, Gereza nalo likatikisika wakati huo vifungo vya wote vikalegezwa na milango ikafunguka.Matendo ya mitume 16:16-35.

Huu ni ukweli usiopingika, nakumbuka kuna wakati ambapo tulikuwa tunaomba kwa ajili ya watu watatu ambao walikuwa wamefungwa na nguvu za giza kwa namna mbalimbali ndipo Mungu akaniambia niache kuomba nianze kusifu.Nilipoanza kusifu nilijishangaa kuona kwamba nikiimba nyimbo hata ambazo sijawahi kuzisikia mithili ya mtu anenaye kwa lugha, nikazidi kupata bubujiko ndipo wale watu wakaanza kufunguliwa kwa namna ya ajabu sana isivyotegemewa.

Kuna wakati mwingine unakuwa na vifungo mbalimbali katika maisha yako, unaona akili ni nzito na huwezi kutatua matatizo au magonjwa mbalimbali labda watoto wako hawafanyi vizuri katika masomo yao na umekata tamaa.Nakusihi hebu ingia kumsifu Mungu na utaona maajabu ambayo haukutegemea.

ii).Kuta za Yeriko zinaondoka katika maisha yako.

Katika mfululizo au hatua ya kumiliki kwa wana Israeli nchi ambayo walikuwa wamepewa na BWANA kuna wakati wakiendelea na safari Mungu aliwaonesha mji wa Yeriko na kuwapa.Lakini haikuwa rahisi kama unavyoweza kufikiria kwani ule mji ulikuwa umefungwa kabisa na kuzungushiwa ukuta mkubwa na imara.



Mungu akasema na Yoshua na kumwambia, “……………………Nanyi mtauzunguka mji huu, watu wote wa vita mkizunguka mji mara moja, fanyeni hivi siku sita…………………..kisha itakuwa watakapopiga hizo pembe za kondoo waume kwa nguvu, nanyi mtakaposikia sauti ya tarumbeta, watu wote watapiga kelele kwa sauti kuu; na ukuta wa mji utaanguka chini palepale, na hao watu watapanda, kila mtu akiendelea mbele kuukabili………………………”.Yoshua 6:1-20.

Sasa anaposema wapige kelele kwa sauti kuu sio kwamba sauti yenye maneno yasiyo na maana ila watoe sifa kwa nguvu sana kushangilia ushindi.Mahali pengine Biblia inasema, Msifuni Mungu kwa kelele za shangwe.KELELE ni sauti isiyo na mpangilio mzuri lakini maneno yatokayo kwenye hiyo sauti yanakuwa na maana halisi.

Mara nyingi unapewa maono mbalimbali ya vitu ambavyo umepewa na Mungu lakini ukitazama huvioni ila unaona ukuta uliovizunguka.Pengine kuna kizuizi cha aina nyingine kinachokufanya usipite na kuyakabili hayo maono.Ninakwambia, “ PIGA KELELE KWA SAUTI  KUU” Umsifu Mungu,Lazima huo ukuta utaanguka tu na hicho kizuizi kitatoka tu maana Mungu wetu ni Mungu ambaye anafanya njia pale pasipokuwa na njia.Kama aliwavusha Israeli kwenye Bahari ya Shamu uwe na uhakika hata katika mapito yako utavuka tu.Usimwache Shetani achukue nafasi kwa kukudanganya na kukukatisha tamaa katika mawazo yako kuwa Mungu hawezi.Yeye ni Alfa na Omega maana yake jinsi alivyofanya jana ndivyo atakavyofanya leo na hata milele yote.Haleluya!!!

iii).Unajazwa kila kitu unachokihitaji.

Duniani hapa wanadamu wote ni wahitaji kwa namna moja au nyingine.Uhitaji ni hali ya kupungukiwa kitu Fulani ambacho ni muhimu sana kwako.Inaweza ikawa ada ya shule, fedha ya matumizi, usafiri, nyumba nzuri, chakula, nafasi ya kazi na mengineyo.Watu wengi wameshindwa kupata vitu wanavyovihitaji kwa kukosea kitu hiki; wanashindwa kusifu kikamilifu kwa vile wanakumbuka uhitaji wao badala ya kumsifu Mungu bila kujali una uhitaji wa namna gani ili Mungu akujaze.Nilikwambia usijaribu kutafakari ukubwa wa tatizo ulivyo wakati unasifu bali tafakari ukubwa wa uweza wa Mungu juu ya hilo tatizo au uhitaji.

Wanasimba hutindikiwa, huona njaa, bali wamtafutao BWANA hawahitaji kitu chochote kilicho chema”.Zaburi 34:10.Hii haimaanishi kuwa hawatatumia vitu vyema.Maana yake hapa ni kuwa hata kama watapungukiwa chochote wana sehemu ya kufanya viongezeke, kwenye kumcha BWANA(katika sifa).

Kuna tofauti kubwa kwa mtu Yule ambaye ameishiwa fedha ya matumizi na anayo ya leo tu na ya kesho hajui ataipata wapi yaani anasubiri muujiza na yule ambaye ingawa ameishiwa leo lakini benki katika akaunti anayo fedha ya kutosha mwaka mzima.Lazima huyu wa pili hawezi kuhangaika au kupoteza muda wake kuanza kuombaomba kwa majirani.

Wakristo wengi wamegeuka kuwa ombaomba kwa watu hata wasiomjua Mungu(wapagani) kwa sababu wameshindwa kutulia na kumsifu Mungu ili awajaze kile wanachokihitaji.Matokeo yake wameingia kwenye gharama ya kupokea vitu kimikataba au kimaagano ambayo ni ya shetani au pengine kupokea vitu ambavyo vimetolewa sadaka kwa miungu, mizimu au kafara.Hebu acha kuwa ombaomba na kumwaibisha Mungu,Mpendwa wa BWANA!! Kumbuka Mungu anacho kila unachohitaji hivyo jukumu lako ni kugeuka na kuanza kumsifu na kumshuhudia Mungu kwa mambo makuu anayoyatenda na hakika atakupa unachokihitaji.Hata kama unasumbuliwa na ugonjwa Fulani hebu uambie kwa imani tulia kimya niweze kumsifu Mungu halafu anza kumsifu Mungu kwa moyo wako wote hakika Mungu atatenda.

iv)Unapewa kushinda na zaidi ya kushinda.

Sifa inatumika pia kama moja ya silaha kuu ya kiroho.Kumbuka vita vyetu kama watu tuliookoka ni vya rohoni kwa sababu maadui tunaopambana nao wapo katika mfumo wa roho katika ulimwengu wa roho maana yake silaha tunazopaswa kuwa nazo ni za rohoni(2wakorintho 10:3-5).Mara nyingi Mungu alipokuwa anawatuma watu wake kwenda kupigana vita silaha kuu aliyowaambia kuitumia ni sifa.Ndivyo ilivyokuwa hata kwa wana wa Israeli kabila la Yuda wakati wanaongozwa na mfalme Yehoshafati.

 “naye alipokwisha kufanya shauri na watu, akawaweka wale watakaomwimbia BWANA na kusifu katika uzuri wa utakatifu, wakitoka mbele ya jeshi na kusema,Mshukuruni BWANA; kwa maana fadhili zake ni za milele.Nao walipoanza kuimba na kusifu, BWANA akawaweka waviziao juu ya wana wa Amoni na Moabu, na wa mlima Seiri, waliokuja juu ya Yuda; nao wakapigwa”.2Mambo ya nyakati 20:21-22.

Na ukisoma sura yote utaona kuwa ilifikia maadui wakaanza kuuana wenyewe kwa wenyewe lakini sababu yake ni sifa.

Ndugu yangu usione maadui wanakuja mbele yako halafu ukaanza kupiga mahesabu ya kujisalimisha hebu piga kelele sema, “NAMSHUKURU BWANA KWA MAANA FADHILI ZAKE NI ZA MILELE”.

Nakuambia iwe wachawi, mizimu, mapepo, majini, waganga wa kienyeji au aina yoyote ile ya mateso hata ya kimwili njaa, magonjwa, ukame, na adui yoyote Yule, usiogope.Maana Mungu wetu hataki kuaibika na unapomsifu juu ya ukuu wake mbele za adui ndipo anataka ajioneshe kwa adui uhalisia wa kile kinachotamkwa na wewe kupitia sifa zako, atakupigania nawe utanyamaza kimya.

Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda”.Warumi 8:37.Ushindi wako hautakuwa wa kawaida utakapochukua hatua ya kumsifu Mungu sawasawa.Tamka mafanikio katika BWANA hata kabla ya kuona mafanikio.Tamka lolote jema ambalo unaamini lipo mbele yako hata kabla hujaliona Mungu akupendaye atakapoiangalia hiyo sifa yako lazima atakujibu tu.

Comments

Popular posts from this blog

NAMNA YA KURUHUSU UTUKUFU (GLORY) WA BWANA KUFANYA JAMBO KATIKA MAISHA YAKO